Bodaboda zinapunguza tatizo la ajira – Lowassa

Lowassa
Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa amesema kuwa bodaboda ni sera ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambayo ina nia ya kusaidia kukabiliana na tatizo la ajira kwa vijana.

Akizungumza katika harambee na uzinduzi wa mfuko wa waendesha pikipiki maarufu mkoani Arusha, Lowassa alisema hiyo ni sera ya CCM kuwakomboa vijana na kuongeza kuwa kitendo cha wafanyabishara wa Arusha kujipanga kusaidia bodaboda ni cha mfano kwa wafanyabishara wengine nchini.
“CCM ni chama kinachotetea wanyonge na nyinyi ni wanyonge mnaohitaji kunyanyuliwa kimaisha, kitendo hiki cha wafanyabishara wa Arusha ni kuunga mkono sera ya chama,” alisema.
Lowasaa alirejea tahadhari yake kuwa tatizo la ajira ni bomu linalosubiri kulipuka.
“Tusipowasaidia vijana kuondokana na tatizo hili, amani itatoweka na ndiyo maana CCM katika Ilani yake ya Uchaguzi imeliweka hilo na pia kulisisitiza katika vikao vyake vya juu mkutano mkuu pamoja na halmashauri Kuu,” alisema.
Arusha ni ngome kuu ya Chadema na vijana ndiyo wafuasi wake lakini tukio hilo limeonekana kama kuwateka vijana hao.
Wafanyabiashara maarufu jiji Arusha wakiongozwa na Mjumbe wa halmashauri Kuu na Diwani wa Mererani, Mathias Manga ndiyo waliyobuni wazo la kuwaanzishia mfuko vijana wa bodaboda.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama Cha waendesha bodaboda mkoani Arusha, Fabian Shayo, alimpongeza Lowassa kwa kuwa msemaji mkuu wa tatizo la ajira kwa vijana na kumuomba asikatishwe tamaa na yanayosemwa.
Katika harambee hiyo zaidi ya Sh. milioni 84 zilipatikana, huku Lowassa pamoja na marafiki zake akichangia Sh. milioni 10 na pikipiki 10.
back to top