Mangula kupokea wanaCCM wapya kutoka vyuo vikuu
Kwa ufupi
MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi( CCM)
Bara, Philip Mangula leo anatarajia kuwasili mkoani Iringa na kufanya
mkutano wa hadhara katika viwanja wa Mwembetogwa mjini hapa huku habari
zikieleza kuwa atapokea wanachama wapya kati ya 400 hadi 500.
Akizungumza na gazeti hili ofisini kwake mjini
hapa, Katibu wa CCM Mkoa wa Iringa, Emanuel Mteming’ombe alisema ziara
ya makamu mwenyekiti huyo ni ya siku mbili na imelenga kukagua uhai wa
chama na utekelezaji wa ilani ya CCM mkoani hapa.
Ziara hii ni ya kwanza kufanyika tangu kuchaguliwa
kwake katika uchaguzi wa chama hicho uliofanyika mwishoni mwa mwaka
jana mkoani Dodoma yalipo makao makuu ya CCM Taifa.
“Makamu atawasili kesho (leo) saa sita mchana hapa
Iringa na akifika kazi yake ya kwanza itakuwa ni kupokea wanachama
wapya wengi wanatoka katika vyuo vikuu vilivyopo hapa mkoani na baada ya
hapo atafanya mkutano wa hadhara katika Viwanja vya Mwembetogwa na
kuzungumza na wananchi,”alisema Mteming’ombe.
Mtemeng’ombe alisema miongoni mwa wanachama
wanaotarajia kujiunga na CCM wengi wanatoka katika vyuo vikuu vilivyopo
mkoani hapa alivyovitaja kuwa ni Mkwawa ,Tumaini, Ruaha (RUCO) na baadhi
yao ni vijana walio katika Manispaa ya Iringa Mjini.
Alisema wanaorudisha kadi kutoka vyama vya
upinzani hutumia utaratibu wa kuwapokea lakini hawakurupuki kuwaingiza
ndani ya chama hadi wanapofundishwa kanuni za chama,maadili na katiba ya
chama na kujiridhisha kuwa wanastahili kuwa wanachama wa CCM.
Alisema sababu za kufanya hivyo ni utaratibu wa
chama wenye lengo la kuhakikisha kila mtu anayeingia ndani ya CCM
anakuwa amepatiwa mafunzo yanayostahili juu ya namna chama kilivyo na
kuahidi kuishi kadri ya kanuni za chama hicho ili wasiwe na utaratibu wa
kuhamahama.
Chama cha Mapinduzi mkoani hapa kimetangaza rasmi
mikakati yake ya kurejesha jimbo na kutishia kuwatimua katika nafasi za
uongozi wenyeviti wa mashina,matawi watakaoshindw a kuonyesha nia ya
kurejesha Jimbo la Iringa Mjini ambalo kwa sasa linashikiliwa na
Mchungaji Peter Msigwa wa Chadema.