WATU 12 raia wa Ethiopia wamehukumiwa na
mahakama ya Wilaya ya Singida, kulipa faini ya Sh100,000 kila mmoja
baada ya kukiri makosa mawili ya kuingia na kuishi ndani ya ardhi ya
Tanzania bila ya kuwa na kibali halali.
Pia mahakama hiyo, imeamuru basi la Kampuni ya
Mtei ya mjini Arusha lililokuwa limebeba Waethiopia hao kukamatwa na
kutaifishwa kuwa mali ya Serikali.
Waethiopia hao ambao wote bado vijana wadogo na
wengine ni wanafunzi wa shule na vyuo, ni pamoja na Ahmed Mohammed
Mahamud, Tazana Walao, Mohammed Osman, Abraham Nirato Shango, Adinan
Abdalah na Alamu Gabresekesie.
Weingine ni Muhidini Sufiani Ahmed, Tasfai Sutatu
Kidisu, Yassin Mohammed Hassan, Afandi Aden Suleiman, Ayele Liranso
Gafuche na Pakala Agore Mancha.
Baada ya mwendesha mashtaka mwanasheria wa
Serikali Ahmed Seif kuwasomea makosa hayo mawili ya kuingia na kuishi
nchini bila ya kuwa na kibali, washtakiwa wote kila mmoja kwa nafasi
yake, walikiri kutenda makosa hayo.
Kabla ya kutolewa kwa adhabu hiyo, Mwanasheria wa
Serikali, Seif, aliiomba mahakama hiyo iwape adhabu kali washtakiwa
ikiwa ni njia moja wapo ya kukomesha vitendo vya wahamiaji haramu
kuingia na kuishi nchini bila ya kuwa na kibali chochote halali.
Akitoa hukumu hiyo, Hakimu Mfawidhi Kiongozi wa
Mahakama ya Wilaya ya Singida, Flora Ndale alisema mahakama yake
imezingatia yale yote yaliyoombwa na upande wa mashtaka na utetezi na
kufikia uamuzi wa kutoa adhabu ya kulipa faini ya Sh100,000 kila
mshtakiwa.
Washtakiwa wote 12 walilipa faini hiyo.
Washtakiwa wote 12 walilipa faini hiyo.
Kwa mujibu wa Mwanasheria wa Serikali Seif,
washtakiwa hao walikamatwa Januari 17, mwaka huu alasiri katika eneo la
Kijiji cha Kititimo nje kidogo ya Mji wa Singida wakiwa wametokea mkoani
Arusha wakidai kwenda Afrika Kusini.