Uongozi wa Chama cha Viziwi Tanzania (CHAVITA) wakiwa kwenye picha ya
pamoja. Kutoka kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Chavita Wilaya ya Ilala
Suleiman Zalala, Gervas Komba (katikati) Katibu, pamoja na Omary Kitingo
ambaye ni Mwanachama (Picha na Joseph Zablon)
MCHAKATO wa kuunda Katiba Mpya bado unaendelea
na sasa upo katika hatua ya uundwaji wa Mabaraza ya Katiba ya Wilaya
yatakayokuwa na jukumu la kuipitia Rasimu ya Katiba. Kazi hiyo
inatarajiwa kuanza Juni mwaka huu.
Pamoja na kuanza kwa mchakato huo wa uundwaji wa
mabaraza ya katiba, wananchi wanaendelea kutoa mapendekezo yao yenye
lengo la kuboresha mchakato huo wa upatikanaji katiba mpya.
Shirika linalojishughulisha na utetezi wa watu
wenye ulemavu la Under The Same Sun ni miongoni mwa wadau wa katiba
waliotoa maoni kuhusu mchakato huo ambapo kwa upande wake linasema
“lingependa kuona Katiba Mpya inaheshimu, kuzitambua na kulinda haki za
Walemavu”.
Meneja Uendeshaji wa Shirika hilo Gamariel Mboya
na Mkurugenzi Mtendaji wake Vicky Ntetema wanasema kwa nyakati tofauti
kuwa Shirika hilo limejikita katika kutetea watu wenye ulemavu wa ngozi
nchini kwa kupitia programu kuu mbili ambazo ni elimu na uhamasishaji.
Kwa kuzingatia majukumu na malengo ya Shirika lao,
wanaona vyema Katiba Mpya ikaboresha haki za kibinadamu za watu wenye
ulemavu wa ngozi na hali za watu wenye ulemavu mbalimbali nchini.
Usawa na haki za Walemavu
Under The Same Sun inataka Katiba Mpya kutambua na kuweka mkazo juu ya haki na usawa kwa watu wenye ulemavu kwa kutambua mahitaji yao maalumu.
Under The Same Sun inataka Katiba Mpya kutambua na kuweka mkazo juu ya haki na usawa kwa watu wenye ulemavu kwa kutambua mahitaji yao maalumu.
“Watu wenye ulemavu wa ngozi wanahitaji visaidizi
katika elimu, visaidizi hivyo ni vikuza maandishi, vitabu vyenye
maandishi makubwa (siyo chini ya font 14), nyongeza ya muda katika
mitihani iliyochapwa kwa mujibu wa mahitaji yao, kutambuliwa kwa
changamoto zao za uoni hafifu pamoja na matatizo ya ngozi,” anafafanua
Gamariel Mboya.
Mboya anapendekeza Katiba ijayo ihakikishe kuwa
Walemavu wa ngozi wanapatiwa tiba sahihi na huduma ya utambuzi wa
viashiria vya saratani ya ngozi na kutibiwa katika hatua za awali.
“Pia ulinzi na usalama kwa watu wenye ulemavu wa
ngozi ni suala linalochafua sura ya taifa kila uchao. Ili kuliondolea
taifa sura hii na kuwafanya watu walemavu wa ngozi waishi kwa amani na
utulivu, tunapendekeza mfumo wa nyumba kumi uwe wa kiserikali,” anasema
na kuendelea;
“Shughuli za upigaji ramli, kuagua, kutambua
wachawi, kuroga wengine, kupandisha cheo, kutajirisha watu, mafanikio
katika biashara, kushinda uchaguzi, mitihani na kutumia viungo vya
binadamu vipigwe marufuku kikatiba,”anasisitiza Mboya.
Wasiyoona na walemavu wa viungo
Watu wenye ulemavu wa kutoona na wale wenye ulemavu wa viungo, wanapaswa kutambuliwa kikatiba kwa kupatiwa mahitaji yao muhimu.
Watu wenye ulemavu wa kutoona na wale wenye ulemavu wa viungo, wanapaswa kutambuliwa kikatiba kwa kupatiwa mahitaji yao muhimu.
Mahitaji ya wasiyoona yameelezwa kuwa ni
urasimishwaji wa maandishi ya nukta nundu (brail) kwenye vitabu,
magazeti, mitihani na maeneo mengine ya kitaaluma na masuala ya habari.