Wassira asema Waislamu ndiyo wachinje

Stephen(1)(1)
Waziri wa Sera, Uratibu na Bunge, Stephen Wassira
Waziri wa Sera, Uratibu na Bunge, Stephen  Wassira, ameunga  mkono kauli  iliyotolewa  na  Mkuu  wa Mkoa  wa  Mwanza, Evarist Ndikilo kwamba suala la uchinjaji wanyama kwa ajili ya biashara liendelee kufanywa na Waislamu.

Wassira alitua mkoani hapa kusuluhisha mgogoro baina ya Waislamu na Wakristo na kutoa msimamo muda mfupi baada ya kufanya kikao na viongozi wa madhehebu ya dini hizo.
Mbali na kauli hiyo, Wassira aliwataka viongozi wa dini waisaidie serikali katika kuhubiri amani nchini.
Alisema kupitia  kikao hicho cha juzi, wajumbe walipendekeza kiundwe chombo maalumu kitakacho kutanisha viongozi wa Kikristo na Waislamu kwa lengo la kuepusha vurugu zinazoweza kusababisha machafuko mkoani hapa.
Alisema chombo hicho siyo lazima kiwe chini ya uongozi wa mkuu wa mkoa na kwamba kitasaidia kufanya mazungumzo kati ya pande hizo kuepuka migogoro.
“Baada ya kukutana na viongozi wa pande zote mbili tumependekeza kwamba suala  la  uchinjaji kwa ajili  ya biashara  liendelee kufanywa na Waislamu;  na kwamba Mkristo anayechinja kwa ajili ya kitoweo nyumbani  kwake  asibughudhiwe,”  alisema  Wassira.
Alisema mbali na hatua hiyo, serikali inaendelea na mazungumzo baina ya viongozi  wa pande zote mbili, ili kuepusha machafuko pamoja na uvunjifu  wa amani.
Waziri Wassira alisema siyo vyema Taifa likafikia  machafuko ama vita kutokana na sababu za imani   za dini.
Hata hivyo, baadhi ya wajumbe wa kikao kupitia  madhehebu ya kikristo walionekana  kupokea  ushauri  huo kwa shingo upande  kwa madai  kuwa  hakuna mwenye uhalali  wa kuchinja kuliko mwingine baina ya Waislamu na wakristo.
Mgogoro baina ya waislamu  na Wakristo uliibuka  mwishoni mwa mwaka jana katika kijiji cha Nyehunge wilayani Sengerema na kusababisha Mkuu wa Mkoa, Ndikilo,  kufanya  mkutano na  wanakijiji  hao kwa kuagiza utaratibu wa Waislamu  kuchinja kwa ajili ya biashara uendelee.
Kwa upande wao, baadhi ya Wakristo walitaka   serikali iruhusu kuwapo kwa maduka ya nyama  ambayo imechinjwa na Wakristo.
CHANZO: NIPASHE
back to top