Mahakama Kuu.
MAHAKAMA Kuu Kitengo cha Biashara, imeipiga
marufuku Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kubomoa wala kuingilia
shughuli za ujenzi wa majengo mawili ya ghorofa yanayojengwa na Kampuni
ya Silverstone Properties Company Ltd, Oysterbay, Dar es Salaam.
Majengo hayo ambayo yameiingiza matatani
halmashauri hiyo, moja linajengwa katika kiwanja namba 321 eneo la
Haile Selassie, lenye urefu wa ghorofa tano na jingine la ghorofa mbili
katika kiwanja namba 288, Toure Road Oysterbay, wilayani Kinondoni,
jijini Dar es Salaam.
Amri hiyo ilitolewa Alhamisi na Jaji, Agathon
Nchimbi kufuatia maombi yaliyowasilishwa mahakamani hapo na wakili wa
kampuni hiyo, Jerome Msemwa wa Kampuni ya Uwakili ya Msemwa &
Company Advocates, chini ya hati ya dharura.
Hati hiyo ya dharura inadai suala hilo linahitaji
hatua za haraka za mahakama kuingilia kati kwa kuwa mjibu maombi hayo
(Jiji) anaelekea kusimamisha shughuli za ujenzi huo kinyume cha sheria
wala sababu yoyote inayoeleweka.
Hati hiyo ya dharura pia inadai kuwa kusudio hilo
la mjibu maombi ni kinyume cha sheria na masharti ya mkataba uendelezaji
na umilikaji wa pamoja wa majengo hayo, baina ya mtoa maombi na mjibu
maombi.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo,
Kamal Jaffar, katika hati ya kiapo chake iliyoambatanishwa katika
maombi hayo namba 4 ya mwaka 2013, kampuni yake iliingia mkataba na
jiji, kujenga na kumiliki kwa ubia majengo hayo. Hata hivyo, anadai kwa
sasa halmashauri hiyo inataka kuifukuza kampuni yake katika mradi huo,
tena bila taarifa wala sababu za kueleweka, kinyume cha mkataba baina
yao.
Katika hoja zake za mdomo mahakamani hapo, Wakili
Msemwa alidai kuna tishio kubwa la mjibu maombi (jiji) kutaka kubomoa
majengo hayo siku za mwisho wa juma (kati ya Jumamosi na Jumapili), siku
ambazo hakuna shughuli za mahakama.
Jaji Nchimbi katika amri hiyo alisema baada ya
kutafakari hiyo za Wakili Msemwa, pamoja na mazingira ya suala hilo,
ameridhika kuwa suala hilo linahitaji hatua za haraka za mahakama
kuingilia katika kwa madhumuni ya haki.
Hivyo aliamuru pande zote hali iendelee kuwa kama
ilivyo katika majengo hayo kama yalivoainishwa katika hati ya maombi,
hadi leo wakati mahakama itakaposikiliza pande zote, huku akiziamuru
pande zote kufika mahakamani hapo leo saa 4:30 asubuhi.