
Wema Sepetu akibubujikwa na machozi baada ya kuondokewa na baba yake mzazi.
Balozi Sepetu alifariki dunia katika Hospitali ya TMJ, Dar alikokuwa
amelazwa kwa matibabu ya ugonjwa wa kisukari na kupooza ambapo
alidondoka hivyo kusababisha mauti yake.Kwa mujibu wa mama Wema, mzee Sepetu alipata tatizo hilo hivi karibuni akiwa Zanzibar.
Balozi Sepetu hadi anapatwa na mauti, alikuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Uwekezaji wa Vitega Uchumi Visiwani Zanzibar.
Mama mzazi wa Wema akiwa na simanzi baada ya kuondokewa na mumewe mzee Sepetu.
MAMA WEMAMama Wema alilisimulia gazeti hili simulizi ya majonzi kinagaubaga kuanzia mwanzo wa kuugua kwa mumewe hadi kifo.
Alisema kuwa bado yupo kwenye hali ya huzuni baada ya kufiwa na mumewe ambaye amedumu naye kwa muda wa miaka mingi kabla ya kupatwa na mauti.
Mama Wema alisema alipokea kwa masikitiko makubwa taarifa za kifo cha mzee Sepetu.
“Ni kama ndoto, mume wangu alipatwa na ‘stroke’ japo alikuwa na tatizo la kisukari.
“Ukweli ni kwamba mume wangu amefariki dunia, ameondoka katika wakati ambao bado nilimhitaji sana, alikuwa baba mzuri anayejua majukumu yake ndani ya familia.
“Tulimpenda, tunampenda lakini Mungu kampenda zaidi, nimeumia sana kuondokewa na mume wangu.
“Nasikitika sana kwani sijawahi kuwa na wakati mgumu kama nilionao sasa,” alisema mama Wema kwa majonzi huku akitiririsha machozi mashavuni.
Jeneza lenye mwili wa marehemu Balozi Sepetu likiwa mbele ya wanafamilia wakati wa kuaga.
Jumapili asubuhi, gazeti hili lilifika nyumbani kwa akina Wema na
kushuhudia watu waliofika mapema msibani hapo wakiwemo marafiki wa staa
huyo, Kajala Masanja na Zamaradi Mketema.Kajala na Zamaradi walikuwa bega kwa bega kuwatia moyo kwa kuondokewa na ‘jemedari’ wao, mzee Sepetu.
Habari za ndani ya familia zilieleza kuwa mazishi yatafanyika leo huko Zanzibar ambapo kwa mujibu wa Wema, alikuwa akisubiriwa baba yao mdogo, Amani Sepetu ambaye alikuwa Afrika Kusini na dada zake wawili waishio ughaibuni.
WEMA ASIMULIA KWA MAJONZI
“Baba yetu alikuwa mtu muhimu sana katika maisha yetu, alikuwa mshauri mkubwa wa familia yetu.
“Kifo cha baba yangu kimenisikitisha sana, ameugua kwa muda mrefu, aliteseka sana lakini hadi anafariki dunia alisisitiza umoja na mshikamano kwa wanandugu wote. Hakika tutamuenzi milele. Kazi ya Mungu haina makosa,” alisema Wema huku akiangua kilio.
WASIFU MFUPI WA MAREHEMU MZEE SEPETU
Amewahi kuwa Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki kati ya mwaka 2001-2006.
Balozi Sepetu amewahi kuwa Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo Visiwani Zanzibar na Naibu Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje miaka ya 70 wakati wa utawala wa Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.
Pia amewahi kuwa Balozi wa Tanzania nchini Urusi tangu mwaka 1982.
Machi 27, mwaka huu, Balozi Sepetu aliteuliwa na Rais wa Zanzibar, Dk. Mohammed Shein, kuendelea kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Uwekezaji Vitega Uchumi Visiwani Zanzibar (ZIPA).
Uongozi wa Global Publishers unatoa pole kwa wanafamilia wote kwa kuondokewa na mzee wao marehemu Balozi Sepetu.