
            
Waziri wa wizara hiyo, Dk Shukuru Kawambwa  PICHA|MAKTABA 
            
Miezi kadhaa imepita sasa tangu ulipozuka 
mjadala mkubwa wa kitaifa kuhusu matokeo mabaya ya mtihani wa kidato cha
 nne wa mwaka 2012. Mengi tuliyasikia na mengine hayakuwekwa bayana hadi
 leo.
Ila kinachojulikana kwa wengi ni kuwa matokeo hayo
 yalibadilishwa, kiasi kwamba alama za ufaulu zimepanda hivyo kutoa 
fursa kwa wahitimu waliofeli kuendelea na masomo ya kidato cha tano au 
hata mafunzo mengine.
Hata hivyo, baadhi ya watu wanahoji kuhusu hatua 
ya uongozi wa siasa kuingilia kati utendaji wa Baraza la Mitihani la 
Taifa (Necta), kwa kuamrisha urekebishaji wa matokeo hayo. Je, hatua 
hiyo ni sahihi? wanauliza.
Aidha, wapo wanaojiuliza kama baraza hilo lina 
nguvu tena ya kusimamia na kutetea uamuzi wake. Kwa watendaji wa baraza,
 bila shaka wana taratibu zao kama taasisi ya kujitathmini na kuangalia 
utendaji wao wa kila siku.
Hata hivyo, mimi siamini kama Katibu Mtendaji wa 
Baraza la Mitihani, Dk Joyce Ndalichako alikurupuka tu siku moja na 
kuamua kubadili viwango vya ufaulu vilivyolalamikiwa na watu wengi.
Bila shaka kwa kutumia wataalamu wake, kuna 
utaratibu wa kitaaluma uliotumika kutathmini mfumo wa utoaji viwango wa 
zamani na hatimaye kutumia mfumo mpya.
Kama taratibu hizi zilifuatwa na zikaleta matokeo 
yale tuliyoyashuhudia, kwa nini baraza lilazimishwe kubadili matokeo? 
Kwa nini matokeo yale yasingechukuliwa kama changamoto ya kufanyia kazi?
Kwa nini tumechagua kupingana na ukweli ulio 
dhahiri, na kulazimisha kuyaona yale tu ambayo tungependa kuyaona hata 
kama hayaakisi hali halisi? Bado najiuliza hivi mwaka huu tutaendelea 
kutumia mfumo mpya au ule wa zamani?
Inawezekana kuwa tukiona hali ni mbaya, tutatumia 
mfumo wa zamani na pale hali itakapokuwa ahueni tena tutatumia mfumo 
mpya. Sasa msimamo wetu kama Taifa ni upi katika elimu?
Jambo jingine kubwa lililoambatana na tukio hili 
lilikuwa ni kuundwa kwa tume maalumu ya kuchunguza hali mbaya ya matokeo
 yale. Cha kushangaza mwaka unakatika majibu ya tume hiyo hayajawekwa 
bayana. Tuliambiwa kuwa maelezo aliyotoa Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, 
Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvi, Bungeni ilikuwa ripoti ya awali.
Ripoti halisi iko wapi na je, Serikali imeshaanza 
kujipanga kwa ajili ya matokeo yajayo, maana muda si mrefu wanafunzi 
watafanya tena mitihani ya kidato cha nne mwaka huu?
Serikali inapaswa kutambua, kuthamini na 
kushirikiana kikamilifu na wadau wengine wa elimu. Kuendelea kuunda tume
 bila kutoa majibu, ni kuwanyima nafasi na haki wadau wengine wa elimu 
ambao nao wanaweza kuchangia kuchukua hatua stahiki za kubadili hali ya 
mambo. Hakuna nchi iliyoendelea bila ya kuwekeza vilivyo katika elimu 
bora. Elimu bora ni pamoja na kuwa na misingi na misimamo ambayo 
haiyumbishwi na hisia za kisiasa.
chanzo;mwananchi.
chanzo;mwananchi.
 
 
