Kinana: Makada wamegeuka mitambo ya kupika majungu

 

  KATIBU Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana amesema baadhi ya makada wa chama hicho, ni mitambo ya kupika majungu hali ambayo inaendeleza makundi.

Kinana alisema hayo juzi wakati akizungumza na viongozi wa chama hicho na wananchi aliposimama kwa muda mkoani hapa, akiwa safarini kuelekea Kigoma ambako atafanya kazi mbalimbali za jamii, ikiwa ni maandalizi ya sherehe za kutimiza miaka 36 ya CCM zitakazoadhimishwa Jumapili ijayo.
“Kuna baadhi ya makada ambao kazi yao ni kuwagombanisha viongozi wao kwa kupikiana majungu, wapo wanaodiriki kutuma hata ujumbe wa simu za mkononi kwa mwenyekiti wa chama kumweleza kuwa katibu fulani hafai,” alisema Kinana.
Alisema fitina hizo zikiendelea zitakidhoofisha chama na kwamba, wenye malalamiko wanatakiwa kuyatoa kwa viongozi wao siyo kuruka kwenda ngazi za juu.
Pia, Kinana aliwataka viongozi kuwa makini kuna watu wanaopika majungu kwa ajili ya kujipatia fedha, kwani hupika majungu na kueleza mbinu watakazotumia kuwanusuru viongozi hao.
“Ili kukinusuru chama lazima wanaCCM tuache majungu, hayajengi! Kiongozi unapoletewa majungu fuatilia ili kujua ukweli, wenye majungu hawana nafasi kwenye ofisi yangu wanafahamu nitawaumbua,” alisema Kinana. Alisema baadhi ya wapika majungu wanafanya hivyo wakiwa na malengo binafsi, hasa uchu wa madaraka.
Alisema amefuatilia na kubaini muda mwingi ndani ya CCM unatumiwa na makada katika malumbano kwa sababu za kupikiana majungu, jambo ambalo alitaka likomeshwe na watakaobainikwa watachukuliwa hatua za nidhamu. Kinana alisema huu siyo wakati wa viongozi wa CCM kulumbana, bali kukijenga chama kiweze kutatua kero za wananchi.
“Nimefuatilia na kugundua kuwa malumbano mengi hayapo kwa malengo ya kutetea masilahi ya wananchi, bali ubinafsi na uchu wa madaraka, tunasema hapana! Huu ni wakati wa kutambua tunatakiwa kujenga chama chetu,” alisema Kinana na kuongeza:
“Vikao vingi vinavyofanyika sasa unakuta siyo kuzungumzia jinsi ya kushughulikia matatizo ya wananchi, bali ni kumshughulikia kada au kiongozi hali hii hatutafika ndiyo maana nasema tunatakiwa kuwa wamoja kwa ajili ya kujenga chama chetu.”
Alisema zamani vikao vya chama viliitishwa kwa mambo ya msingi ya kujadiliwa, lakini hivi sasa vikiitishwa vinakuwa vya kushughulikia mtu.
“Binafsi wananijua sina muda wa kuhangaika na mambo ya nani kafanya nini, maana kama nataka kufuatilia taarifa za kiongozi najua utaratibu upi unafaa kujua kinachoendelea, siyo huu wa kupewa taarifa tu na mtu,” alisema Kinana.
back to top